Monday, January 18, 2021

MTI WENYE MATUNDA UNAPIGWA MAWE

Watu wengi tumekuwa na kasumba ya kutokupongeza jitihada za wenzetu kwa maana ya vijana wenzetu na watu wazima ambao wamepiga hatua za maendeleo kwa kiasi fulani. Unakuta watu wanapiga stori kwenye vijiwe wakisema mtu yule anajisikia sana, amekuwa na roho mbaya, anatupita bila kutusalimia wakati jamaa wakati bado hajatoboa alikuwa mwana kinyama.
Wengine wanaanza kutengeneza scenario za kuwa hata mafanikio yake sio halali, haiwezekani atoboi kirahisi hivi itakuwa amejiunganisha na mambo ya freemason, atakuwa amewatoa ndugu zake sadaka na nk.
Yote yananenwa kwa sababu ya chuki, roho isiyokubali na kuamini kuwa mapambano ya maisha yanaweza kumpa hatua mtu kufikia malengo na ndoto zake. Bahati mbaya sana akifanikiwa Mtanzania ndio itakuwa habarï kubwa yakusemwa kwa mtazamo hasi, tumewaona wanamuziki wetu hapa nchini wamepambana wameutoa muziki kwenye vumbi lakini unakuta kuna mtu yuko swekeni huko anamponda anamsema vibaya, wakati huo huo anamsifia mwimbaji wa Nigeria, USA na nchi zingine kama vile wanawafahamu sana...
Hii inatokea kwenye maeneo yote kwenye maisha yetu, iwe kwenye biashara nje na muziki, madukani, kwenye soka, kwenye mafanikio ya dini zetu hasa watumishi wa Mungu, kwenye siasa, kwenye kazi za maofisini na maeneo mengine, utakuta watu wanasema huyu asingekuwa baba yake asingekuwa hapo, sasa tujiulize baba yako angekuwa kwenye nafasi ya kukunyanyua asingefanya ivo. Na asipofanya hivyo si ataonekana mpuuzi na asiye na akili.
Ukiona unaandamwa sana na maneno jua wewe una kitu cha ziada, watu wakawaida huwa hawazungumzwi maana hawana kitu chakuwafanya watu kuwazungumzia.
Huwezi kwenda kuchuma matunda kwenye mchongoma, na shida ya mchongoma kama mti una faida moja au mbili ambazo pia utazipata kwenye mchungwa, mwembe, mpera na mpeazi pia, unatoa kivuli labda na mbao ambazo pia sio mbao bora, kumbuka pia mwembe na miti mingine inatoa kivuli na mbao ambazo zinaweza zisiwe bora pia ila inatoa.
Sasa kama una sifa za mchongoma nani atakuzungumzia, maana sifa ulizo nazo kila mtu anazo, sifa za kawaida. lakini mti wa matunda unapigwa mawe kwa sababu una sifa ya ziada, wakati wa jua, wakati wa mvua na wakati wa hali zote watu wataufikia ule mti, watakula matunda, watajikinga mvua au jua nk.
Ndivyo ilivyo kwa watu wenye sifa za ziada, watasemwa vibaya vijiweni, wakipewa tuzo huko mataifani watapokelewa kwa nderemo na vifijo, kila mmoja atajifanya anampenda huyo shujaa.
Hivyo basi ni vyema kuilinda miti yenye matunda maana inatufaa sote, wapo watu wameajiliwa kupitia mafanikio ya mtu ambae ametutangulia, mfano mzuri ni Diamond ni zaidi ya familia hata hamsini wanakula kwa sababu ya matunda ya kazï yake. Hakika mti wenye matunda hupigwa mawe
Mgema Moses
mgemamoses@gmail.com

1 comment: