Thursday, February 11, 2021

NI KWA SABABU YA KILICHO KWENYE WALETI NA POCHI YAKO TU WALA SIO KINGINE

Wakati unafanya vizuri utakuwa mzuri na mwenye heshima kubwa sana mbele za watu. Ukiwa na fedha, kipaji ambacho kinakupa matokeo chanya na kuwagusa watu wengi kwenye jamii, ukiwa tajiri, kiongozi  kama mbunge na hadhi zingine kwenye jamii hasa jamii za kiafrika, utaitwa kila aina ya majina mazuri, tajiri, mweshiwa, kiongozi, doni, kaka, mkubwa, mzee hata kama una umri wa miaka chini ya kumi ila kwa sababu wanachokiita majina yote mazuri hata wewe unaheshimika.

Sio ajabu Tanzania mgonjwa kunyimwa hela ya matibabu na baadae watu kutoa mamilioni ya shilingi wakati umefumba kinywa na huzungumzi tena, jeza la kifahari, kaburi na chakula cha haja na sifa kedekede.

Ni rahisi mtoto kukosa ada ya shule baada ya kuvuja jasho na damu akitafuta ada ya shule tena ada ya shule za serikali kwa majirani, ndugu na jamaa akakosa kwa kunyimwa huku watu wakija na sababu kedekede za unajua mwanangu sina hata hela nimepeleka shamba, mama yangu ambae ni bibi yako alikuwa anaumwa na pole nyingi ningekuwa nayo ningekupa hela wakati huo asilimia kubwa wakijigeuza kuwa mamotivational na mainspirational speakers kukuita jiniazi na unatakiwa kupambana ili kufikia ndoto yako. Muda mfupi ukiondoka watu walewale ambao walikosa ada ya shule za serikali unakuta wanachangia malaki ya pesa kwenye harusi ya mshikaji wao au kwenda kuweka heshima bar na washikaji huku wakipeana stori, na stori zenyewe ni za yule yatima aliyepita mchana kuomba msaada kwa ajili ya ada na mahitaji ya shule ili kupigania ndoto zake.

Ni somo gumu sana lakini kuwa makini na watu wa nchi hii au ulimwengu huu, usipende kusifiwa na kuvimba kichwa kwa kuitwa majina yenye hadhi ukaona umefika, kumbuka kuna watu wanakuita majina mazuri huku wakiitazama waletï na pochi yako, uishimiwa wako ni kwa sababu ya dolla, misimbazi na pounds unazomiliki, heshima unayopewa si ya kwako ni kile ulicho nacho basï.

Hadhï yako ni kwa sababu ya kile ulichonacho kuanzia kwenye nyumba ya Baba yako maiti haitazikwa mpaka ufike hata kama uko ulaya na corona imefunga mipaka ya nchi unahitaji kuunga unga ili ufike kwenu mwandugembe ulipo msiba tena wa mtoto mdogo kabisa, ukoo utakutambua, kijiji mpaka tarafa watakuita majina ya heshima na hadhi na wewe utavimba kichwa, kwenye baadhi ya nyumba za ibada hata kama unatenda dhambi ambayo wengine wakifanya wanapigwa na fagio la chuma, wewe watachekacheka nakutengeneza mazingira ambayo kosa lako litaonekana la kawaida na vifungu vya Biblia vitatumika kukulinda na kukutetea USIHUKUMU USIJE ''UKAHUKUMIWA, YULE ANAE JIONA MWEMA AWE WA KWANZA KUMSIMAMISHA HUYU NK.''Sio wewe ni fedha, mali na utajiri wako.

Jitahidi kufanya mambo ya msingi, fanya ambayo unapaswa kufanya, usifanye jambo kwa sababu unafikiri una kundi kubwa la watu nyuma yako wanakupenda na kukuelewa hapana, wengi wao ni wasengenyaji na watoa taarifa zako pindi utakapojikwaa na utajiri ukaisha, pale kipaji chako hakitawagombanisha watu wanaojiita watu wa connection, mawakala na watu wa menejimenti muda huo watakuwa wametimua mbio.

Fanya kila unalolifanya huku ukikumbuka kuwa yule kijana mdogo aliyekosa ada kipindi kile nakazunguka mtaani, kwa ndugu kwa rafiki wa marehemu mama au Baba wakasema hawana hela na kuambulia kumpa pole, leo wanamwita mweshiwa baada ya yeye kuvuja jasho bila msaada leo wamegeuka nakuwa washuhudiaji na wenye kujigamba wakisema huyu amekuwa tunamwona, tumemsaidia sana Baba yake alipofariki sisi ndiyo tuĺisimamia masomo yake mpaka leo ni daktari.

Unapokuwa na mali wewe ni mtamu na unastahili kila jina zuri hakika, ila kumbuka wanaokusema vyema mchana katika giza wanakuita mpumbavu huna akili kazi kutumia mali na pesa vibaya, wengine hata hawajawahi kukushauri lakini wakiwa vijiweni kutwa kusema huyu jamaa hashauriki, tunamshauri sana lakini wapi kumbe masikini ya Mungu hata kukushauri hawajawahi kukuambia ukweli, kuwa makini ndugu yangu.....
Usirubunike na maneno matamu ya walimwengu, jenga msingi bora wa maisha yako, usikubali kurubuniwa kwa maneno mazuri ya watu kwa sababu ya utajiri wako, fanya jambo muhimu kwa wakati sahihi, usipende kuifurahisha kila nafsi ya mtu bali ishi wewe kwa utaratibu wako.
Mungu akupe kujua watu wakweli mbele yako na waongo ili kuyaweka maisha yako salama kesho.
Mgema Moses
0715366003/0755632375

No comments:

Post a Comment