Thursday, June 9, 2022

Historia ya binti tajiri aliyeamua kwa dhati ya moyo kuigeuza ndoto yake kuwa kweli.
Katika ya jiji la Mwanza, mji ulio kando mwa Ziwa Victoria, anazaliwa binti mmoja toka familia masikini ya Mzee Anthony Masaga kwenye mitaa maarufu ya mabatini.

Ni familia duni iliyokosa nuru ya maisha bora, wameamua kuishi kama wanasubiri kifo kije kikawapumzishe, sio Baba, mama hata watoto wa kiume na wakike ambao walikuwa na namna ya kuiokomboa familia yao kutoka katika umasikini uliotapakaa kizazi kimoja hadi kizazi kingine...

Stori ya Baba kwa watoto wake ilikuwa ni kila siku kusema, nilizaliwa katika familia masikini, Babu yenu hajuwahi kumiliki hata mfano wa Baiskeli, hatukujua kitanda wala mfano wa godoro, tulilala chini, tulilala njaa mpaka umri wangu huu sikuwahi kuamini kuwa kutoka kwenye familia au ukoo wetu kuna siku tutalala kwenye nyumba ya bati mbali ya nyumba ya block.....
Kati ya watoto saba wa mzee Anthony Masaga, alikuwepo binti mmoja, aliyepewa jina la kizungu la Victoria kwa mfanano wa jina la ziwa lililopo Jijini mwanza, alikuwa ni mtoto pekee aliyekuwa na jina la tofauti, wengine waliitwa majina ya asili ya kabila la mzee huyo, manumbu, Michembe, madaso, Yumbu, Nyanzobe, kabula na hatimaye mtoto wa mwisho akipata jina la Victoria.

Nyumba ya chumba kimoja na sebule ilitosha kukusanya idadi ya watu tisa wakike na wa kiume, familia ilinuka umasikini kuanzia fikra, mpaka mwonekano wa nje, stori yenye kuhuzunisha na kusikitisha sana, kwa sababu Baba, mama na hata watoto wao wa kwanza waliamini umasikini ni haki na halali yao.

Shule kwao ilikuwa ni hadithi walizozisikia kwa majirani zao kama ilivyo kwa vyakula kama wali, pilau na hata wakati mwingine hata ugali ilikuwa ni taabu kwao, michembe ndiyo ilikuwa chakula kikuu kwa familia ya mzee Anthony Masaga pale Mabatini Jijini Mwanza.

Miaka mingi baada ya kupita tangu Victoria alipozaliwa, umri ulikuwa umesogea kiasi cha kutambua maumivu ya ufukara katika familia yao, kulala njaa, kukosa mavazi, kukosa huduma kama za watoto wenzake, zilitengeneza unyonge na maumivu makali sana kwa mtoto Victoria.

Mara nyingi alimuuliza mama yake kwa nini mimi sends shule kama kina Pendo, Kina Joshua na watoto wengine, mama aliishia kusema, sisi ni masikini hatuna uwezo wa kukupeleka shule ndiyo maana hata kaka na dada zako hawajasoma, tena sisi kwetu, yaani kwenye ukoo wa Baba yako na ukoo wetu hakuna hata mmoja aliyewahi kwenda hata shule ya awali....

Maisha yale na hadithi za mama yake alikuwa akizielewa na kuamini kwamba kuna watu wenye haki ya kupata elimu, kuishi maisha mazuri, na wengine wameandikiwa maisha duni, ufukara na kukosa baadhi ya mambo ya msingi kama kwenda shule, kula vizuri na kuishi kwenye nyumba za kifahari....

Maisha hayo aliishi kwa kujaribu kuyaamini lakini, sehemu ya ubongo wake ilikuwa haimpi kuamini kama ni kweli, hali ambayo ilimfanya kutokuridhika na majibu ya mama yake, alijaribu kuwauliza wenzake, huku moyoni mwake akitamani kuwa kama wao...

Miaka kumi baada ya kuzaliwa, ufahamu na uelewa kiasi unazidi kushika ufahamu wake, akili yake moja, inakataa kukubaliana na mama yake, lakini kila akikumbuka anawaona ndugu zake wakiwa hawana ramani yeyote, hawajawahi kuwa sehemu ya watu waliofanikiwa kwenda shuleni, akikumbuka anaemwambia kuwa elimu na mambo mengine ni kwa baadhi ya familia ni mama yake mzazi moyo unamwambia ni kweli elimu sio haki yako Victoria wewe ni masikini kwa sababu mmeandikiwa kuwa masikini.

No comments:

Post a Comment